Wednesday, June 6, 2012

RC Kagera atangaza kiama cha wahamiaji haramu

Ng'ombe wa wafugaji wanaohusishwa na uhamiaji haramu wakiwa katika malisho Wilayani Karagwe
Aina ya ng'ombe wanaofugwa Mkoa wa Kagera
MKUU wa Mkoa wa Kagera kanali mstaafu Fabian Massawe amesema wakati wowote itafanyika oparesheni kubwa ya kuwaondoa wahamiaji haramu katika wilaya zote aliosema ni tishio kubwa la usalama wa nchi.

Akizungumza juzi katika kikao cha Kamati ya ushauri ya Mkoa(RCC)kanali Massawe alisema zoezi hilo litavihusisha vikosi mbalimbali vya ulinzi na usalama na kuwaonya wenyeji watakaowahifadhi wahamiaji hao.

Kwa mujibu wa Massawe Mkoa wa Kagera una jumla ya wahamiaji haramu 35,000 aliodai wanafahamika kwa majina wakiwemo wafugaji na kuwa makundi hayo ni tishio kubwa la usalama wa mkoa na taifa.

"kuna wahamiaji haramu elfu thelathini na tano tunaowafahamu kwa majina na sehemu walipojificha,oparesheni kubwa ya kuwaondoa itaanza wakati wowote kwani ni tishio kubwa la usalama"alisema Massawe.

Aidha Massawe alisema kuwa tayari mkoa umeomba kiasi cha shilingi milioni mia sita kwa ajili ya oparesheni hiyo na kuwa kufumbia macho suala la wahamiaji haramu unaweza kuwa mwanzo wa kukaribisha makundi ya waasi kutoka nchi jirani na kujificha katika nchi yetu.

Hata hivyo Mkuu wa Mkoa wa Kagera kanali mstaafu Fabian Massawe alionyesha wasi wasi wa kuwadhibiti wahamiaji hao wasirudi tena baada ya kubainika kuwa baadhi ya wananchi wanahusika na kuwahifadhi wahamiaji hao.

No comments:

Post a Comment