Thursday, September 27, 2012

Marufuku ya kuchimba ‘dawa’yashika kasi


Baadhi ya abiria wakinunua bidhaa mbalimbali baada ya kuchimba 'dawa'katika kituo cha Gairo Mkoani Dodoma
 Phinias Bashaya,Morogoro
AGIZO la Waziri wa Uchukuzi Dokta Harrison Mwakyembe la kupiga marufuku abiria wanaosafiri na mabasi  kujisitiri vichakani limenza kushika kasi kwa mabasi yanayotoa huduma ya usafiri maeneo mbalimbali mikoani.

Katika agizo lake alilolitoa miezi michache iliyopita Bungeni,Waziri Mwakyembe alisema utekelezaji  wa marufuku hiyo utaanza Septemba mosi kwa mabasi yote yanayosafirisha abiria kwenda mikoa mbalimbali nchini.

Mwandishi wa habari ambaye amesafiri kwa nyakati  tofauti na mabasi yanayotoa huduma ya usafiri kati ya mikoa ya Kanda ya ziwa na jijini Dar es salaam ameshuhudia jinsi yanavyokwepa kuwasimamaisha abiria vichakani na badala yake kuegesha katika vituo maalumu vya kuchimba dawa.

Aidha katika moja ya basi la kampuni  inayosafirisha abiria kutoka Bukoba kwenda Dar es salaam alisikika mmoja wa wahudumu wa basi hilo akiwatahadharisha abiria wake kuwa hawataweza kusimama vichakani kwani wanaogopa kupigwa faini.

Mhudumu huyo alikuwa akiwahamasisha abiria wake wachimbe’dawa’katika kituo maalumu kilichopo nje kidogo ya mji wa Kahama na kuwa wasingeweza kusimama tena mpaka watakapofika kituo kingine kwa ajili hiyo.

Hata hivyo baadhi ya abiria walilalamikia uongozi wa Kampuni hiyo kuwa na maegesho ya magari yao mjini Morogoro eneo walilodai vyoo vilikuwa vichafu na kutaka kupewa maelezo ya basi hilo kutofikia kituo cha Mabasi cha Msanvu  usiku wakati likisubiri kuendelea na safari alfajili.

Kwa mujibu wa malalamiko ya baadhi ya abiria walidai pamoja na vyoo kuwa vichafu,pia vilikuwa uchochoroni  maeneo yasiyokuwa na mwanga hali iliyokuwa inahatarisha maisha yao hasa akina mama na watoto.

Wakati akitoa agizo hilo Bungeni Waziri Mwakyembe alisema kitendo cha abiria kujisitiri vichakani kinachangia uharibifu wa mazingira na hata kuhatarisha usalama wa maisha ya abiria wanaoweza kukumbana na wanyama wakali.

Pia alisema kuchimba dawa vichakani ni kitendo kilichipitwa na wakati na pia kinawadhalilisha abiria ambao hulazimika kuvua nguo hadharani hali aliyosema Serikali haiwezi kuendelea kuifumbia macho.



No comments:

Post a Comment