Thursday, September 20, 2012

watendaji wa Kata na vijiji Karagwe walalamikiwa

Enzi zile Kanali Mstaafu Fabian Massawe akiwa Mkuu wa Wilaya ya Karagwe,kabla ya kupanda daraja na kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera.Hapa alikuwa akikabidhi trekta lililotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa wananchi wa Wilaya hiyo

Phinias Bashaya,Karagwe
BAADHI ya wananchi wa Wilaya ya Karagwe wamewalalamikia maofisa watendaji wa vijiji na kata kwa kuwatoza zaidi ya shilingi 30,000 kama gharama za kuandikiwa barua za utambulisho kwenda katika ofisi na taasisi mbalimbali.

Adha hiyo imewakumba zaidi wananchi wanaohitaji barua za utambulisho kutoka kwa maofisa hao ili waweze kupewa malipo ya fidia ya kupisha ujenzi wa barabaraya kiwango cha lami kutoka Kyaka hadi Bugene.

Kwa mujibu wa maelezo ya baadhi ya wananchi ambao tayari wametozwa kiasi hicho cha fedha,walisema huojiwa kwanza kama wametoa michango ya ujenzi wa shule za sekondari za Kata na Zahanati kabla ya kunadikiwa barua za utambulisho.

Walisema mwananchi anayeshindwa kuonyesha stakabadhi za michango mbambali hulazimika kutozwa kuanzia shilingi elfu thelathini ili aweze kuandikiwa barua ya kumtambulisha ili apewe malipo yake.

Pia wananchi wanaohitaji barua za utambulisho kwa ajili ya kuwadhamini ndugu zao katika vituo vya polisi,mahakama na wanaotaka kufungua akaunti za akiba katika Benki hutakiwa kuonyesha stakabadhi za michango au kulipa kiasi icho cha fedha vinginevyo hapewi barua ya utambulisho.

“Hii ni aina mpya ya ufisadi nimeandikiwa barua ya utambulisho na Mtendaji wa Kata baada ya kulipa kiasi cha shilingi elfu thelathini nilihitaji kwenda kumdhamini ndugu yangu kituo cha Polisi”alisema mmoja wa wananchi kutoka Kata ya Bugene.

Baadhi ya wananchi waliolalamika walikiri kuwa hawajawahi kutoa michango ya shughuli za maendeleo kwa zaidi ya mwaka huku wakidai kuwa kiasi cha fedha wanayotozwa ni kubwa mno huku wakionyesha wasiwasi wa matumizi ya fedha hizo pamoja na kuwa wanapewa stakabadhi za malipo.

Pamoja na walalamikaji kuomba majina yao yahifadhiwe kwa hofu ya kupata msukosuko baadaye,mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Kishao Justus Daniel alisema utaraibu huo unatumika katika Kata nyingi za Wilaya hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Karagwe Bosco Ndunguru alisema suala la kutoza wananchi fedha kwa ajili ya kuandikiwa barua halipo na kuwataka walalamikaji wafike ofisini kwake na kumtajia majina ya wahusika ili aweze kuwachukulia hatua.

Alisema yuko tayari kurudishia fedha za wananchi endapo watendaji wanaohusika na tuhuma hizo watajulikana  na kuwa ofisi yake iko tayari kuidhinisha barua hizo bila malipo kwani wanalipwa mshahara kwa ajili ya kuwatumikia wananchi.

No comments:

Post a Comment