Wednesday, September 19, 2012

RC Kagera amnyang'anya mbunge shule na kuikabidhi kwa wananchi


Mkuu wa Mkoa wa Kagera Kanali Mstaafu Fabian Massawe(aliyeruka juu)akifurahia na wananchi wa Kata ya Katoke kucheza ngoma baada ya kuwakabidhi shule iliyokuwa na mgogoro kati yao na mbunge wa zamani wa Muleba Kaskazini Ruth Msafiri
Baadhi ya wananchi wa Katoke wakielekea katika shule iliyokabidhiwa jana na Mkuu wa Mkoa wa Kagera
MKUU wa Mkoa wa Kagera Kanali Mstaafu Fabian Massawe ameingilia kati mgogoro wa shule iliyodaiwa kumilikiwa na Mbunge wa zamani wa Jimbo la Muleba Kaskazini Ruth Msafiri na kuamua kuikabidhi kwa wananchi.

Mgogoro wa shule ya sekondari ya wasichana ya Ruth Msafiri umedumu kwa zaidi ya miaka miwili na ulioibuka baada ya Ruth kubwagwa katika kura za maoni (CCM)na hivyo kushindwa kutetea nafasi yake na baadaye kudai shule hiyo ni mali yake binafsi.

Shule hiyo imejengwa katika Kitongoji cha Kimbugu,Kata ya Katoke na inadaiwa ilianzishwa na mbunge huyo wakati wa kipindi chake cha uwakilishi baada ya kupewa ardhi na Serikali ya Kijiji kwa makubaliano kuwa iwe ya wananchi wa Kata hiyo.

Pia mgogoro wa sekondari hiyo mapema mwaka huu uliibukia katika Baraza la Madiwani wa Wilaya ya Muleba baada ya tume iliyoundwa kubaini kuwa  Ruth alipewa ekali arobaini na serikali ya kijiji na kuanza kutafuta michango ya ujenzi kwa niaba ya wananchi.

Kwa mujibu wa tume iliyoundwa na Baraza la Madiwani miongoni mwa waliochangia ni Rais wa Jakaya Kikwete aliyetoa mabati mia tatu,mfuko wa maendeleo ya jimbo 3,000,000,benk ya NMB 5,000,000 NA Wizara ya Malisili na Utalii 6,000,000.

Kabla ya Kanali Massawe kukabidhi shule hiyo kwa wananchi juzi,Februari 20,2012 alitembelea kijiji cha Katoke na kufanya mkutano wa hadhara na wananchi na kupewa maelezo ya mgogoro huo.

Baadaye aliwaagiza wananchi kupitia ngazi mbalimbali za kisheria kuanzia kijiji,Baraza la Kata na Baraza la Madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Muleba ili kuridhia kama shule hiyo inastahili kuwa mali ya wananchi.

Kwa mujibu wa Kanali Massawe ameridhika na hatua zilizofikiwa na juzi aliamua kukabidhi shule hiyo kwa wananchi na kuwataka waendeleze ujenzi kwa ajili ya kupokea wanafunzi watakaochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani.

Baada ya kukabidhi shule hiyo alifanya uhamasishaji na kupatikana zaidi ya shilingi milioni mbili,huku wananchi wakihaidi kutoa mchango wa  mawe,mchanga saruji na mbao na kumhaidi kuwa msingi wa vyumba vitatu utakuwa umekamilika kufikia mwezi Januari.

Pamoja na kuhudhuriwa na kundi kubwa la wananchi,makabidhiano ya shule hiyo pia yalishuhudiwa na Mkuu wa Wilaya ya Muleba  Limbres Kipuyo na viongozi wengine wa Serikali.

Hata hivyo Ruth Msafiri hakuweza kupatikana kutoa maoni yake kufuatia hatua iliyochukuliwa na Serikali ya kukabidhi shule hiyo kwa wananchi ambayo awali alidai ni mali yake binafsi.

No comments:

Post a Comment