Wednesday, August 15, 2012

Sheria yadaiwa kuwabagua walemavu wa akili

Mtetezi wa Haki za Watu wenye Ulemavu na Rais wa Shirika la Kutetea Haki za Binadamu(POTA)Idrisa Masalu akitoa mada katika semina ya kutetea haki za walemavu wa akili iliyofanyika mjini Bukoba
Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kagera Rebeca Gwambasa akifungua semina
Washiriki wa semina
Picha ya pamoja na mgeni Rasmi
Mtaalamu wa kitengo cha watoto wenye ulemavu wa akili kutoka Bunazi Wilayani Missenye Mwl Gervase Anatory akitoa mchango wake wakati wa semina
Phinias Bashaya,Bukoba
SHERIA ya watu wenye ulemavu imetajwa kuwabagua watu wenye ulemavu wa akili baada ya haki zao kutofikiwa kwa urahisi tofauti na walemavu wengine huku sheria ikishindwa kulitaja moja kwa moja kundi hilo.

Hayo yamebainishwa katika semina iliyoandaliwa na Chama kwa Ajili ya Watu wenye Ulemavu wa Akili(TAMH)na kuwakutanisha wataalamu wa watu wenye ulemavu wa akili kutoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa Kagera.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa chama hicho Anacret Rugaihuruza watu wenye ulemavu wa akili wana mahitaji makubwa zaidi ya wenzao na sheria ilitakiwa kufafanua haki zao bila kujumuishwa moja kwa moja katika sheria ya jumla ya haki za walemavu.

Alisema chama hicho pamoja na jukumu la kuwasemea walemavu wa akili ni muhimu jamii kutambua kuwa hata walemavu wa kundi hilo wana haki ya kupata mahitaji mengine kama kuoa na kuwa na familia.

Katika semina hiyo iliyofadhiliwa na Shirika la The Foundation for Civil Society,Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kagera Rebeca Gwambasa alikiri sheria ya walemavu kuwa na mapungufu  yanayolitenga kundi la walemavu wa akili.

“Katika haki za walemavu kundi la walemavu wa akili halifikiwi na haki hizo inaonekana wakati sheria inatungwa makundi yote hayakushirikishwa hata hivyo Serikali iko tayari kupokea ushauri”alisema Gwambasa

Miongoni mwa washiriki wa semina hiyo Gervase Anatory ambaye ni mtaalamu wa Kitengo cha watoto wenye ulemavu wa akili Bunazi Wilayani Missenye alisema hata elimu jumuishi inayowachanganya kundi hilo na wasio na ulemavu bado haiwasaidii kutokana na kuwepo vitendo vya unyanyapaa.

Alisema watoto wenye ulemavu wa akili wanapochanganywa na wengine tatizo lao linakuwa kubwa zaidi na kuwa jamii inatakiwa kuwa na mapenzi mema kwa walemavu na kuwasaidia kupata mahitaji mbalimbali.

Naye mshauri wa watu wenye ulemavu ambaye pia ni Rais wa Shirika la Kutetea haki za binadamu(POTA)Idrisa Massalu alisema umefika wakati wa kutengeneza sehemu maalumu 'Camps'kwa ajili ya kundi hilo kwani hukosa mwelekeo wanapomaliza masomo yao.

Pia wanachama na viongozi wa chama hicho wakati wa semina hiyo watajifunza usimamizi na udhibiti wa fedha na kuandaa mpango mkakati utakaotekelezeka.




No comments:

Post a Comment